Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kupitia kitengo cha maliasili na uhifadhi wa mazingira inaendelea kuwaasa wananchi wake kuchukua tahadhari dhidi ya wanyama hatarishi kama vile mamba,viboko na nyoka wanaopatikana kwa wingi kando kando ya vyanzo vya maji.
Akizungumza na wananchi wa kata ya Ngoma ambapo wamekuwa wakidhibiti wanyama pori aina ya mamba mara kadhaa Afisa wanyama pori wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Ndugu Zebedayo Timotheo amewaasa wananchi kuchukua tahadhari katika maeneo hatarishi yenye viashiria vya uwepo wa wanyama hao kwa kuzingatia kuwa Ukerewe ni kisiwa na wengi wao wanapatikana kwenye maji.
Sambamba na elimu ya kujilinda dhidi ya wanyama hatarishi Afisa wanyama pori amesema kitengo cha maliasili kinaendelea kuchukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na wanyamapori hao ikiwemo kutoa elimu ya uhifadhi endelevu,elimu ya kujikinga na kujilinda dhidi ya wanyama hatarishi, kufanya doria za mara kwa mara,ujenzi wa vizimba (crocodile enclosure) kwa ajili ya kupunguza migongano baina ya wanyama pori na wananchi.
Goodluck J.Mtigandi ni Mkuu wa kitengo cha maliasili na uhifadhi wa mazingira Ukerewe yeye amewaasa wananchi wanaojishughulisha na uvuvi kutumia vyombo salama na sahihi na wapende kwenda maeneo ya ziwa kwa makundi hasa nyakati za jioni,usiku na asubuhi sana huku akitoa pole kwa wahanga wote walioathiriwa na wanyamapori hao kwa namna mbalimbali.
Julius Magoma ni mkazi wa kijiji cha Nantare anaushukuru uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kwa ushirikiano mzuri na wananchi kwa kuwa wepesi kufika kwenye eneo la tukio punde wanapopata taarifa ya uwepo wa wanyama hatarishi.
Ikumbukwe kwamba tayari wananchi wawili ndani ya mwaka huu 2026 wamepoteza maisha kwa kujeruhiwa na mamba ndani ya kata ya Ngoma katika kijiji cha Nantare na Muluseni.
Copyright ©2022 Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe . All rights reserved.