Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Ndugu Vincent Augustino Mbua ametoa taarifa ya mapokezi ya watumishi ajira mpya 2026 kuwa tayari wamepokelewa wote kwa 100%.
Akizungumza wakati wa baraza la madiwani kujadili mapendekezo ya mpango na bajeti ya Halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Mkurugenzi Mbua amesema Halmashauri yake ilipangiwa jumla ya watumishi ajira mpya 152 wa kada mbalimbali (afya 108, elimu 25 na Kada nyingine 19 ) ikiwa ni utekelezaji wa miongoni mwa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan ndani ya siku 100 madarakani baada ya kushinda uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 29,2025.
Ameongeza kuwa hadi kufikia jana Januari 28,2026 jumla ya watumishi ajira mpya 152 walikuwa wamesharipoti kazini na kufanya zoezi la mapokezi kufikia 100%.
" Kwa niaba menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe natoa shukrani za dhati kwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wetu Mhe.Samia Suluhu Hassan .Kabla ya ujio wa watumishi hawa tulikuwa na upungufu wa 67%.Ujio wao unakwenda kupunguza changamoto hiyo na kuleta ufanisi katika utoaji wa huduma mbalimbali ndani ya Ukerewe."
Nae Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mhe.Ramadhan Salum Mazige amepongeza serikali kwa kuikumbuka Ukerewe kwa kuleta ajira mpya hao huku akiwasihi wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita .
Suzana Mtaki ni mkazi wa kata ya Nkilizya yeye anasema anafuraha kubwa sana kusikia idadi hiyo ya watumishi wapya huku akiiomba Halmashauri kuboresha mazingira ya kiutumishi ili watumishi wadumu,wasitamani kwenda kwingine.
Copyright ©2022 Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe . All rights reserved.