Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Cde.Christopher Ngubiagai amewasihi wanaUkerewe wote kuwa na utamaduni wa kupanda na kutunza miti ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan katika kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa 27 Januari kila mwaka.
Ameyasema hayo nyakati tofauti akiwa katika eneo la kitalu cha miche ya miti kilichopo Halmashauri na shule ya sekondari Nakoza iliyopo ndani ya kata ya Kagera kijiji cha Kagera ambapo jumla ya miti 500 imepandwa shuleni hapo.
Nae Mkuu wa kitengo cha maliasili na uhifadhi wa mazingira Wilaya ya Ukerewe ndugu Goodluck Mtigandi amesema kwa kushirikiana na wakala wa misitu Tanzania (TFS) -Ukerewe jumla ya miche ya miti 1500 aina ya mikalibea,misila na misadulela imepandwa maeneo mbalimbali ndani ya Wilaya hiyo ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za serikali katika masuala ya utunzaji wa mazingira.
Aidha Cde. Ngubiagai ameongeza kuwa zipo faida nyingi za kupanda na kutunza miti ikiwa ni pamoja na kupambana na mmomonyoko wa ardhi,kuleta mvua, shughuli za ujenzi sambamba na kuzalisha nishati ya kupikia.
James Aloyce ni mhifadhi wa misitu Wilaya ya Ukerewe yeye anasema TFS wataendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kwa kutoa elimu na miche ya miti bure .
Gabriel Zacharia ni mwanafunzi katika shule ya sekondari Nakoza ameahidi kuwa balozi mzuri wa utunzaji wa mazingira kupitia elimu ya utunzaji wa mazingira waliopata shuleni hapo.
" Naomba wananchi wote tupande miti na kuiitunza,tukumbuke kauli mbiu ya mwaka huu inasema Uzalendo ni kutunza mazingira, shiriki kupanda miti."
Copyright ©2022 Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe . All rights reserved.